Utafiti: Watanzania wana wasiwasi kuhusu mashambulizi

Matokeo ya utafiti uliofanywa na shirika la kijamii la Twaweza yanaonyesha zaidi ya 80% ya Watanzania wanaona nchi yao iko salama kutoka kwa vitendo vya makundi yenye itikadi kali.
Utafiti huo wa maoni ulifanywa kati ya mwezi Septemba na Oktoba mwaka huu ukitaka kujua mtazamo wa wananchi juu ya hali ya vitendo vya itikadi kali nchini.
Kwa mujibu wa utafiti huo, ingawa wananchi wengi wanajihisi kuwa salama, takribani asilimia 56 wana wasiwasi juu ya vitisho vya mashambuliz dhidi ya Tanzania katika siku zijazo.
Hata hivyo Meja Jenerali Venansi Mabeo, ambaye ni mkuu wa usalama katika Jeshi la Ulinzi la Wananchi la Tanzania ameondoa wasiwasi huo na kusema hali ya usalama si ya kutia shaka.
Wakizungumzia sababu zinazowashawishi watu wengi kuvutiwa na itikadi hizi, wananchi wengi wamesema ukosefu wa ajira, utawala mbovu pamoja na kukatishwa tamaa na mifumo ya serikali ni mambo yanayoongoza katika ushawishi huo
Kwa upande mwingine, wananchi katika ripoti hiyo wamesema wanapendelea zaidi njia ya kijeshi kuliko ya mazungumzo katika kupambana na vikundi hivi vyenye itikadi kali
Huku zaidi ya asilimia 90 wakionyesha kuridhishwa kwao na vyombo vya ulinzi na usalama na kusema wana Imani kwamba vinaweza kuwalinda dhidi ya vitisho vya mashambulizi
Mkurugenzi Mtendaji wa Twaweza Aidan Eyakuze amesema hata kama utafiti huu unahusu hisia pekee za wananchi, unasaidia pia katika kutoa picha ya juhudi za serikali katika kuimarisha hali ya usalama miongoni mwa wananchi.
Mwandishi wa BBC Sammy Awami anasema tangu shambulio la ubalozi wa Marekani jijini Dar es Salaam mnamo mwaka 1998, Tanzania imeonekana kukwepa balaa la mashambulizi ya kigaidi.
Ripoti hiyo ya Twaweza inasema Tanzania imo katika nafasi nzuri ya kutafuta njia mbadala za kushughulikia tatizo hili linalogonga vichwa vya mataifa mengi duniani

Comments